C
Sala ya Mordekai
17a Ndipo Mordekai alimsihi BWANA, akizikumbuka kazi zote BWANA, akasema: 17b Ee BWANA, BWANA, mfalme Mwenyezi; ulimwengu wote u katika uweza wako, wala hakuna awezaye kukupinga ukipenda kuwaokoa Israeli. 17c Maana Wewe umeviumba mbingu na nchi, na vitu vyote vya ajabu vilivyopo chini ya mbingu, nawe ndiwe BWANA wa vyote wala hakuna awezaye kushindana nawe, BWANA. 17d Wewe unajua yote. Unajua ya kuwa si kwa jeuri, wala kwa kiburi, nilikataa kuinama mbele ya Hamani mwenye makuu. Hakika, kwa ajili ya wokovu wa Israeli ningekuwa tayari hata kuzibusu nyayo za miguu yake. 17e Ila nilifanya hayo nisitangulize utukufu wa binadamu mbele ya utukufu wa Mungu. Sitamsujudia yeyote la Wewe, BWANA wangu, wala sikatai kwa kiburi. 17f Basi, sasa. Ee BWANA, Mungu, Mfalme, Mungu wa Abrahamu, uwaachilie watu wako; maana macho ya watu wanatuvizia ili kutuangamiza, nao wanatafuta kuuharibu urithi ambao umekuwa wako tangu milele. 17g Usilidharau fungu lako ulilojikombolea katika nchi ya Misri. 17h #Kut 3:6 h Yasikie maombi yangu uurehemu urithi wako, ugeuze matanga yetu yawe karamu, ili tuishi na kuliimbia jina lako, Ee BWANA; wala usiiharibu midomo yao wanaokuhimidi, Ee BWANA. 17i Na Israeli wote walilia sana, maana kufa kulikuwapo mbele ya macho yao.
Sala ya Esta
17j Malkia Esta naye alimkimbilia BWANA, akishikwa na uchungu wa mauti. Akazivua nguo zake za fahari akavaa nguo za huzuni na kilio, na badala ya manukato mazuri alijitia majivu na samadi kichwani; akajinyenyekeza mwili wake, hata mahali pa mapambo ya furaha alijifunika wa nywele zake zilizofumuliwa. Akamwomba BWANA wa Israeli, akisema: 17k BWANA wangu, Wewe peke yako u Mfalme wetu. Unisaidie mimi nilie mkiwa, wala sina msaidizi mwingine ila Wewe; maana hatari yangu imo mkononi mwangu. 17l Tangu nilipozaliwa katika kabila ya jamaa yangu, nimesikia ya kuwa Wewe, BWANA, ulimchagua Israeli katika mataifa yote, na baba zetu katika jamaa zao, kuwa urithi wa daima, ukawatimilizia yote uliyoyaahidi. 17m Na sasa tumetenda dhambi mbele zako nawe umetutia mikononi mwa adui zetu, kwa sababu tumeitukuza miungu yao. Ee BWANA, Wewe ndiwe mwenye haki. 17n Wala haiwatoshi ya kuwa sisi tumo katika uchungu wa kufungwa, ila wamepeana mikono, wao na sanamu zao, kuondoa sheria iliyotoka kinywani mwako, na kuuharibu urithi wako, na kuziba midomo yao wanaokuhimidi, na kuuzimisha utukufu wa nyumba yako na madhabahu yako, 17o na kuvifumbua vinywa vya mataifa waisifu miungu ya uongo na kuwaadhimisha daima wafalme wa kibinadamu. 17p Ee BWANA, usiwape wasio miungu fimbo yako ya kifalme, wala wasitucheke katika maanguko yetu, bali uligeuze shauri lao juu yao wenyewe, na kuwaonya kwa adhabu yake yeye aliyetuanzia mambo hayo. 17q Utukumbuke, Ee BWANA; ujifunue wakati wa taabu yetu; unipe moyo thabiti, Ee Mfalme wa mingu na BWANA wa milki zote. 17r #Ydt 9:13 s Unitie kinywani mwangu maneno ya kufaa mbele ya simba, ukaugeuza moyo wake apate kumchukia yule anayepigana nasi, ili akomeshwe pamoja na wote wenye nia moja naye. 17s Lakini utuokoe sisi kwa mkono wako; unisaidie mimi niliye peke yangu, bila msaidizi mwingine ila Wewe, BWANA. 17t Wewe unajua yote. Unajua ya kuwa naichukia fahari ya waovu, na kukikirihi kitanda chake asiyetahiriwa na cha kila mgeni. 17u Unajua ninavyolazimishwa, na jinsi ninavyoichukia ishara ya cheo changu iliyopo kichwani pangu siku ninazojionesha mbele ya watu. 17v #Dan 1:8; Ydt 12:2 w Naichukia kama nguo iliyotiwa unajisi, wala siivai ninapokaa faraghani. Tena, mimi, mjakazi wako sijala mezani pa Hamani, wala kuhudhuri kwenye karamu yake, wala kunywa divai ya sadaka. 17w Mimi mjakazi wako sijajua furaha tangu siku niliyoletwa hapa hata sasa, ila katika Wewe, BWANA Mungu wa Abrahamu. 17x Ee Mungu, uweza wako ni juu ya yote; isikie sauti yao wasio na tumaini, utuokoe mikononi mwao wafanyao maovu, uniokoe katika hofu yangu.