Methali 11
BHNTLK

Methali 11

11
1Mizani ya udanganyifu#11:1 Mizani ya udanganyifu …: Msemo huu unarudiwa katika maandishi ya Sheria (Lawi 19:35-36; Kumb 25:13-16) na katika maandishi ya kinabii (Hos 12:8; Amo 8:5-6; Mika 6:10-11). Taz pia Meth 16:11; 20:10,23. ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu,
lakini matumizi ya kipimo halali ni furaha kwake.
2Kiburi huandamana na fedheha,
lakini kwa watu wanyenyekevu mna hekima.#11:2 Kiburi …wanyenyekevu mna hekima: Kuwa na kiburi au majivuno huweza kumfanya mtu akamdharau Mungu (3:34), akapuuza sheria ya Mungu na badala ya kumtegemea Mungu akategemea tu nguvu zake mwenyewe, akaangamia (Isa 14:11-14). Kuwa mnyenyekevu na kuwa na hekima huenda pamoja.
3Unyofu wa watu wema huwaongoza,
upotovu wa wenye hila huwaangamiza.
4Utajiri haufai kitu siku ya ghadhabu,
lakini uadilifu huokoa kutoka kifo.
5Uadilifu wa watu wanyofu huinyosha njia yao,
lakini waovu huanguka kwa uovu wao wenyewe.
6Uadilifu wa wanyofu huwaokoa na hatari,
lakini wafitini hunaswa kwa tamaa zao wenyewe.
7Mwovu akifa tumaini lake nalo hutoweka;
tazamio la asiyemcha Mungu huishia patupu.
8Mtu mnyofu huokolewa katika shida,
na mwovu huingia humo badala yake.
9Asiyemcha Mungu huangamiza wengine kwa mdomo wake,
lakini mwadilifu huokolewa kwa maarifa yake.
10Waadilifu wakipata fanaka mji hushangilia,
na waovu wakiangamia watu hupiga vigelegele.
11Mji hufanikishwa kwa baraka za wanyofu,
lakini huangamizwa kwa mdomo wa waovu.
12Anayemdharau jirani yake hana akili,
mtu mwenye busara hukaa kimya.
13Apitapitaye akichongea hutoa siri,
lakini anayeaminika rohoni huficha siri.
14Pasipo na uongozi taifa huanguka,
penye washauri wengi pana usalama.
15Anayemdhamini mgeni atakuja juta,
lakini anayechukia mambo ya dhamana yu salama.
16Mwanamke mwema huheshimiwa,
mwanamume mwenye bidii hutajirika.#11:16 Mwanamume …hutajirika: Tafsiri yamkini ya makala ngumu. Tafsiri nyingine: “Watu wakatili … hutajirika”.
17Mtu mkarimu hufaidika yeye mwenyewe,
lakini mtu mkatili hujiumiza mwenyewe.
18Faida anayopata mwovu ni ya uongo,
lakini atendaye mema hakika atapata faida ya kweli.
19Mtu anayepania kuwa mwadilifu ataishi,
lakini anayechagua kutenda maovu atakufa.#11:19 Atakufa: Yaani, atakufa kabla ya wakati wake.
20Wenye nia mbaya ni chukizo kwa Mwenyezi-Mungu,
lakini wenye mwenendo mwema ni furaha yake.
21Hakika mwovu hataepa kuadhibiwa,
lakini waadilifu wataokolewa.
22Mwanamke mzuri asiye na akili,
ni kama pete ya dhahabu puani mwa nguruwe.
23Matazamio ya waadilifu yana matokeo mema;
tamaa za waovu huishia katika ghadhabu.
24Atoaye kwa ukarimu huzidi kutajirika;
lakini bahili huzidi kudidimia katika umaskini.
25Mtu mkarimu atafanikishwa,
amnyweshaye mwingine maji naye atanyweshwa.
26Watu humlaani afichaye nafaka,#11:26 … humlaani afichaye nafaka: Yamkini yahusu wanaoficha nafaka kungojea waiuze kwa bei kubwa wakati wa shida. Ling Yobu 29:13; Amo 8:5.
lakini humtakia baraka mwenye kuiuza.
27Atafutaye kutenda mema hupata fadhili,
lakini atafutaye kutenda maovu atapatwa na maovu.#11:27 Atapatwa na maovu: Yaani, maovu anayofanyia wengine ndio hayohayo atakayofanyiwa. Ling Esta 7:10.
28Anayetegemea mali zake ataanguka,
lakini mwadilifu atastawi kama jani bichi.
29Anayeivunja nyumba yake ataambua upepo.
Mpumbavu atakuwa mtumwa wa wenye hekima.
30Matendo ya mwadilifu huleta uhai,
lakini uhalifu huuondoa uhai.
31Ikiwa mwadilifu hupata tuzo hapa duniani,
hakika mwovu na mwenye dhambi atapatilizwa.

Copyright The Bible Society of Tanzania, 1993

The Bible Society of Kenya 1993

Learn More About Biblia Habari Njema: Toleo la Kujifunza