Zaburi 143
BHNTLK

Zaburi 143

143
Sala ya kuomba msaada
(Zaburi ya Daudi)
1Usikie sala yangu, ee Mwenyezi-Mungu!
Ulitegee sikio ombi langu
maana wewe ni mwaminifu;
unijibu kwa sababu ya uadilifu wako.#143:1 Mwaminifu …uadilifu wako: Mwandishi hapa anataka kusema kwamba Mungu anaweza kuaminika na kwamba yeye hutenda yaliyo sawa kulingana na agano lake kwa watu wake.
2Usinitie hukumuni mimi mtumishi wako,
maana hakuna yeyote aliye mwadilifu#143:2 Hakuna yeyote aliye mwadilifu: Au, “hakuna yeyote asiye na hatia”. Kwa hiyo Mwanazaburi anaomba ahurumiwe na sio apatiwe haki yake. Maneno hayo yanafanana na Rom 3:20 na Gal 2:16. mbele yako.
3Maadui zangu wamenifuatia;
wameniangusha chini kabisa
wameniketisha gizani kama mtu aliyekufa zamani.
4Nimevunjika moyo kabisa;
nimekufa ganzi kwa ajili ya woga.
5Nakumbuka siku zilizopita;
natafakari juu ya yote uliyotenda,
nawaza na kuwazua juu ya matendo yako.
6Nakunyoshea mikono yangu kuomba;
nina kiu yako kama nchi kavu isiyo na maji.
7Ee Mwenyezi-Mungu, unijibu haraka;
maana nimekata tamaa kabisa!
Usijifiche mbali nami,
nisije nikawa kama wale washukao kwa wafu.
8Asubuhi#143:8 Asubuhi: Wakati wa matumaini mapya baada ya usiku wa giza la kukata tamaa. unioneshe fadhili zako,
maana nimekuwekea tumaini langu.
Unifundishe mwenendo wa kufuata,
maana nakuelekezea ombi la moyo wangu.
9Uniokoe, ee Mwenyezi-Mungu, kutoka maadui zangu,
maana kwako nakimbilia usalama.
10Unifundishe kutimiza matakwa yako,
maana wewe ni Mungu wangu!
Roho yako nzuri iniongoze katika njia sawa.#143:10 Njia sawa: Au, “njia iliyo salama”.
11Unifadhili, ee Mwenyezi-Mungu, kwa hisani yako,
uniondoe katika taabu kwa sababu ya uadilifu wako.
12Kwa sababu ya fadhili zako uwakomeshe maadui zangu,
uwaangamize wote wanaonidhulumu;
maana mimi ni mtumishi wako.

Copyright The Bible Society of Tanzania, 1993

The Bible Society of Kenya 1993

Learn More About Biblia Habari Njema: Toleo la Kujifunza